vote

Katibu CCM atimuliwa kwa ubadhirifu







Geita

KATIBU Msaidizi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Wilaya ya Geita amevuliwa madaraka na ofisi yake kufungwa baada ya kutuhumiwa kujihusisha na ubadhirifu wa Sh milioni sita za chama hicho.



Kwa muda mrefu, katibu huyo, Patrick Kusaga, amekuwa akidaiwa kulindwa na baadhi ya viongozi wa ngazi za juu wilayani hapa wanaowania ubunge wa jimbo la Geita.




Katibu huyo alikumbwa na adhabu hiyo baada ya kikao kamati ya siasa ya CCM wilayani kufikia uamuzi huo mjini hapa, juzi.




Kusaga anatuhumiwa 'kutafuna' mamilioni hayo ya fedha yaliyotokana na kodi za pango.




Akizungumza na waandishi wa habari, Katibu Mwenezi wa CCM wilaya hapa, Jonathan Masele, alisema mbali ya kufanya ubadhirifu huo, Kusaga pia amekuwa akionyesha dharau kwa viongozi wenzake.




Masele aliongeza kuwa kamati ya siasa ya wilaya imekuwa ikimwita mara kwa mara ili kuzungumzia tuhuma zake, lakini amekuwa akiwatolea majibu ya kejeli, jambo ambalo limesababisha kumng'oa madarakani.




“Tumefikia maamuzi haya kutokana na katibu huyu msaidizi kujiona yeye ni zaidi ya wenzake na kujipa madaraka makubwa, amehusika na upotevu wa shilingi milioni sita za kodi. Kutokana na hayo, kamati ya siasa ya wilaya imemwita mara kadhaa, lakini ameshindwa kutii wito na amekuwa akitutolea lugha za kejeli kuwa sisi hatuwezi kumfanya chochote kwa kuwa anawakubwa wanaomlinda,” alisema na kuongeza:




“Kamati ya siasa ya wilaya hatumtaki, labda mkoa au makao makuu wampeleke wanakojua wao, lakini hapa hatumhitaji, anasababisha chama kiyumbe na anaweza kusababisha tulikose hili jimbo la Geita, tumeamua kufunga na ofisi yake hapa, tunasubiri kuletewa mtu mwingine, huyu hafai kabisa kuwa hata balozi kwa ufisadi wake. Kadi za CCM tunaziuza shilingi 300, lakini yeye anaziuza shilingi 540 kinyume na utaratibu.”




 Hata hivyo, Kusaga alipoulizwa na gazeti hili alisema hajui lolote kuhusu suala hilo na kwamba alikuwa njiani akitokea wilayani Butiama, Mara kwenye msiba wa mtoto wa Mwalimu Julius Nyerere, John Nyerere.




“Hizo tuhuma mimi sizijui na sijaitwa na tunapoongea nipo Mwanza natoka Butiama kwenye msiba wa mtoto wa Mwalimu Nyerere," alisema Kusaga.




Taarifa kutoka ofisi ya CCM wilayani hapa pia zilidokeza kuwa huenda Katibu wa wilaya naye akatimuliwa kutokana na tuhumza za kushirikiana na huyo msaidizi wake katika matumizi mabaya ya madaraka.




 ''Nikuambie ni muda mrefu hawa watu wamekuwa wanatusumbua sana, ukiwaita hawaji, lakini katika kuhakikisha tunafanya vizuri katika uchaguzi ujao ni vyema hawa watu waondoke tuletewe wengine, vinginevyo watatuharibia uchaguzi mkuu," alisema mmoja wa makada wa CCM wilayani hapa aliyeomba kutotajwa jina.





Share this article :

Post a Comment

 
Support : GUDMUSICS BLOG | Gm Template | Gm Template
Copyright © 2015. NGOWI HABARII - All Rights Reserved
Template Created by 0756494700 Published by GM Template
Proudly powered by gudmusics blog