vote

Waandishi watakiwa kuandika habari za uchunguzi.






Bariadi.

WAANDISHI wa habari mkoani Simiyu wametakiwa kujikita zaidi kuandika habari za uchunguzi badala ya kuzama kwenye habari za matukio pekee.

Changamoto hiyo ilitolewa na Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Ponsian Nyami, wakati akimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Simiyu, Eraston Mbwilo, katika hafla ya kukutana na wadau wa habari mkoani wa Simiyu, juzi.

Alisema jamii kwa sasa inakabiliwa na changamoto nyingi ambazo zinaweza kuwekwa wazi katika vyombo vya habari na kupatiwa ufumbuzi katika muda mwafaka kwa kutumia njia za magazeti, redio, runinga na mitandao ya kijamii.

“Vyombo vya habari ni muhimu sana katika jamii yetu, hasa katika kuchochea shughuli za maendeleo hapa nchini, hususan kwenye maeneo ambayo kwa sasa yako nyuma kielimu kama mkoa wetu wa Simiyu,” alisema.

Aliongeza kuwa ni vizuri kwa waandishi wa habari kuandika habari za kina, hasa makala juu ya changamoto zilizoko kulingana na maeneo yao kuliko ilivyo sasa ambapo walio wengi huandika
habari za matukio.

“Sasa ni vizuri mkajikita katika kuandika habari za kiuchunguzi zaidi katika jamii inayowazunguka kulingana na maeneo mliyopo, hasa changamoto, lakini mlio wengi mnajikita sana katika habari za matukio, hasa yale ambayo yanatishia hata kufanya shughuli za maendeleo,” alisema.

Hata hivyo, alitumia muda huo kuwapongeza waandishi wa habari wa mkoa huo kwa kutangaza na kuhamasisha wananchi kuchangamkia na kutumia fursa zilizopo kama vile ufugaji, kilimo, biashara, madini, elimu, afya, utawala na mazingira katika kuinua na kuboresha hali ya maisha yao.

Kwa upande wake, mdau wa habari mkoani Simiyu, Martine Moga, alisema tasnia ya habari ni muhimili muhimu katika nchi kwa ajili ya kuelimisha na kuhabarisha umma.

''Waandishi wa habari ni sehemu muhimu sana katika kulijenga taifa, waandishi wa habari wana uwezo mkubwa wa kubomoa au kujenga taifa, hivyo wanahabari mjikite zaidi katika habari zenye ukweli na siyo kupotosha umma kwani Watanzania wanategemea sana tasnia ya habari," alisema Moga.

Katika risala ya waandishi wa habari wa mkoa huo iliyosomwa na Samwel Mwanga, walisisitiza kuwepo kwa ushirikiano imara wa kati yajamii, vyombo vya habari na wadau wa habari kwa jumla katika kujenga na kuinua mkoa wa Simiyu na taifa lenye amani na utulivu.

‘Sisi waandishi wa habari wa mkoa wa Simiyu tunasisitiza kuwepo kwa ushirikiano wa kutosha kati yetu na wadau wa habari kwa lengo la kujenga na kuinua zaidi mkoa wetu wa Simiyu na kujenga taifa lenye amani na utulivu,” ilisema sehemu ya risala hiyo.
Share this article :

Post a Comment

 
Support : GUDMUSICS BLOG | Gm Template | Gm Template
Copyright © 2015. NGOWI HABARII - All Rights Reserved
Template Created by 0756494700 Published by GM Template
Proudly powered by gudmusics blog