Mkurugenzi Mtendaji wa kituo cha sheria na Haki za Binadamu(LHRC) Dr Helen Kijo-Bisimba.
Mkurugenzi Mtendaji wa kituo cha sheria na Haki za Binadamu(LHRC) Dr Helen Kijo Bisimba ameitaka serikali pamoja na watendaji wake kufanya maamuzi kwa njia ya ushirikishwaji ili kuepuka migongano inayopelekea kutokea migomo huku wananchi ndio wanao athirika sana katika migomo hiyo.
Kauli hiyo inafuatia kutokea mgomo mkubwa wa madereva uliotokea nchi nzima siku ya ijumaa iliyopita ambapo madereva walipinga kurudi shule kila leseni zao zinapokwisha huku ajira zao zikiwa hazina mikataba pamoja na maslahi yao kubanwa na waajiri.
Akizungumza na kituo kimoja cha redio asubuhi yah hii Dr. Bisimba amesema migongano pamoja na kutoeleawa kati serikali na wananchi inatokana na serikali kushindwa kuwashirikisha wadau au wananchi katika mambo mbalimbali ili kufikia muafaka wa jambo wanalopanga.
Aidha, Bisimba amesema muda wa serikali kudhani kwamba wanaweza kufanyia wananchi maamuzi umepitwa, hivyo viongozi kadhaa kukutana maofisini na kujiamulia pasipo ushirikishwaji wa jambo husika kwa wananchi matokeo yake yanakuwa ndio hii migomo tunayo iona.
Akizungumzia kuhusu kutengua maamuzi mara baada ya jambo linalopngwa na serikali kushindwa kwa njia ya migomo amesema kuwa hiyo inaonesha kuwa serikali ni dhaifu isiyo na mipango mikakati dhidi ya mambo yanayo anzishwa.
Kwa upande wake Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka akizungumzia kuhusu kutengua maamuzi ya kuwataka madereva kusoma amesema, serikali ikihusisha mawaziri husika italiangalia suala hilo huku akisisitiza kufanya kikao na viongozi wa madereva pamoja na kupitia mikataba yao ambayo imekuwa ikilalamikiwa.
Katika hatua nyingine Dr. Bisimba ameishauri serikali kuandaa mipango kwa kufanya majadiliano kwa kushirikisha wahusika ili kuepuka migomo inayowagharimu wananchi kila wakati.
Post a Comment